
Katika hali isiyo ya kawaida mshambuliaji wa Yanga Amisi Tambwe jana alipewa mpira feki na mwamuzi John Fannuel aliyechezesha mchezo wa jana (January 21, 2016) kati ya Yanga dhidi ya Majimaji kwenye uwanja wa taifa, Dar es Salaam.
Tambwe alifunga magoli matatu kwenye mchezo huo ambao Yanga walipata ushindi wa mago 5-0 dhidi ya Majimaji. Kwa mujibu wa kanuni za soka, mchezaji anayefunga magoli zaidi ya mawili hupewa mpira mmoja kati ya ile ambayo ilitumika kwenye mchezo husika.

Lakini jana mambo yalikuwa tofauti, wakati mwamuzi wa mchezo huo anamkabidhi Tambwe mpira wake, mshambuliaji huyo alishtuka kwamba mpira aliopewa haukuwa miongoni mwa ile iliyotumika kwenye mchezo wao dhidi ya Majimaji. Alipodai mpira uliotumika kuchezea mchezo husika mwamuzi alitia ngumu.
Baada ya kugundua ujanja huo uliofanywa na mwamuzi, mtandao huu ulimfuata mwamuzi huyo na kumuuliza kwanini Tambwe hakukabidhiwa mpira uliotumika kwenye mechi ya Yanga na Majimaji? Mwamuzi huyo alisema huo ndiyo utaratibu uliopo na kama kuna maswali zaidi basi waulizwe wasimamizi wa ligi.

Mbali na hayo, Tambwe alisema hat trick yake inamwendea moja kwa moja mchumba wake. Hat-trick hiyo ni ya pili kwa Tambwe msimu huu, nyota huyo alipiga bao tatu kwa mara kwanza kwenye msimu huu December 19, 2015 wakati Yanga ilipocheza na Stand United na ku-dedicate bao hizo tatu kwa mtoto wake.
Kwenye mchezo kati ya Yanga dhidi ya Stand United Tambwe alikabidhiwa mpira uliotumika kwenye mchezo huzika lakini cha kushangaza ni mpira aliopewa jana ambao haukuwa miongoni mwa ile inayotumiwa kwenye ligi msimu huu.
