Usiku wa Mei 24, 2017 tuzo za VPL zilitolewa kwa wachezaji, timu na waamuzi waliofanya vizuri katika kipindi chote cha msimu wa 2016/2017 ambapo zilitolewa tuzo takribani 15 kwenda kwa watu mbalimbali.
Washindi wa nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi ni Azam FC ambao wamepewa kiasi cha pesa cha shilingi milioni 24.
Kagera Sugar wakashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi na kujishindia shilingi milioni 30.
Simba imekamata nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi na kuzawadiwa shilingi milioni 42.
Mabingwa wa ligi guu Tanzania bara ni Yanga ambao wametwaa kitita cha shilingi milioni 84.
Tuzo ya timu yenye nidhamu imekwanda kwa Mwadui FC ya Shinyanga na kuzawadiwa shilingi milioni 17.5
Tuzo ya mfungaji bora imechukuliwa na wachezaji wawili Simon Msuva (Yanga) na Abdulrahman Musa (Ruvu Shooting) ambao kila mmoja alifunga magoli 14 kwenye msiu wa ligi.
Mwamuzi bora wa msimu ameshinda Elly Sassi wa Dar es Salaam akiwashinda Shomari Lawi (Kigoma) na Hans Mabena (Tanga). Mwamuzi bora amezawadiwa shilingi milioni 5.8.
Mecky Maxime ameshinda tuzo ya kocha bora wa msimu baada ya kuisaidia Kagera Sugar kumaliza katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi. Maxime amewazidi Joseph Omog (Simba) na Etiene Ndayiragije (Mbao FC).
Tuzo ya mchezaji bora kijana (U20) imepewa jina la Ismail Khalfani Mrisho aliyekuwa mchezaji wa Mbao ambaye alifariki uwanjani akiitumikia timu yake kwenye mashindano ya ligi ya vijana, tuzo hii ameshinda Shabani Idd Chilunda wa Azam FC. Mshindi amezawadiwa shilingi milioni 4.
Tuzo ya heshima ikaenda kwa Kitwana Manara mchezaji wa zamani wa Yanga na timu ya taifa ya Tanzania.
Tuzo ya golikipa bora wa msimu imechukuliwa na Aishi Manula wa Azam FC akiwashinda Juma Kaseja (Kagera Sugar) na Chaima (Mbeya City).
Mbaraka Yusuf (Kagera Sugar) ameshinda tuzo ya mchezaji bora chipukizi.
Tuzo ya mchezaji bora wa kigeni anaecheza ligi kuu Tanzania bara imekwenda kwa Haruna Niyonzima kiungo wa Yanga raia wa Rwanda.
Goli bora la msimu ameshinda Shiza Kichuya, goli lake alilifunga wakati Simba ikicheza dhidi ya Yanga.
Mchezaji bora wa VPL 2016/2017 ikaenda kwa Mohamed Hussein Tshabalala mlinzi wa kushoto wa Simba na timu ya taifa.