Fainali ya kombe la Azam Sports Federation Cup kati ya Simba dhidi ya Mbao ilikuwa ni ya kiwango cha juu na ilistahili kuitwa fainali inayotoa mshindi anaekwenda kushiriki michuano ya kimataifa na kuiwakilisha nchi.
Ukiachana na uhondo wa fainali hiyo, kulikuwa na burudani nyingine nje ya uwanja ambapo inawezekana kwa wale ambao hawakuwepo uwanjani iliwapita au hata wale waliokuwepo uwanjani walipitwa kutokana na sehemu walipokuwa wamekaa.
Shaffihdauda.co.tz inakuletea matukio sita yaliyo bamba nje ya uwanja na kuwa kiburudisho kwa wengine .
Farasi
![]()
Farasi aliyetumika kupambana na mashabiki waliokuwa sio waungwana wakati wa mchezo wa fainali ya kombe la shirikisho (Azam Sports Federation Cup) alikuwa kivutio kikubwa kwa mashabiki wengine waliokuwa uwanjani wakishuhudia fainali hiyo iliyozikutanisha Simba na Mbao.
Farasi huyo aliyekuwa akiongozwa na askari wa jeshi la polisi alikuwa akikabiliana na mashabiki ambao sio wastaarabu waliokuwa wakitoka kwenye maeneo yao na kushuka chini kwenye maeneo ya kukimbilia.
Mara kadhaa polisi akisaidiwa na Farasi aliwakimbiza mashabiki na kuwapeleka kwa askari wengine ambao walikuwa wanawakamata mashabiki kwa urahisi na kuwaingiza ndani ya magari yao na kupunguza ghasia ambayo ingeweza kutokea na kuharibu mchezo.
Kitendo cha Farasi kupambana na mashabiki wasio wastaarabu kilikuwa ni kivutio kwa mashabiki wengine ambao ni wastaarabu na mara kadhaa walionekana wakishangilia mambo yaliyokuwa yakifanywa na Farasi.
Raia wa kigeni
![]()
Kwa mujibu wa takwimu unaambiwa mchezo wa soka ndio mchezo unaoongoza kwa kupendwa ulimwenguni halafu michezo mingine inafuata nyuma.
Mchezo wa soka unakutanisha watu wa rika tofauti, makabila, dini, itikakadi, mataifa na mambo mengine kibao, kwenye mchezo wa fainali ya ASFC, kuna raia wengi wa kigeni walijitokeza kushuhudia mxhezo huo ambapo walikuwa kivutio pia kwa mashabiki waliokuwepo uwanjani kwa sababu walionekana wakishangaa namna ushangiliaji wa wabongo hususan kikundi cha mashabiki wa Mbao waliokuwa wakishangilia kwa style ya aina yake.
Mashabiki wa Mbao
![]()
Hawa unaweza kuwafananisha na wale mashabiki wa Sports Extra Ndondo Cup kutokana na ubunifu wao wa hali ya juu kwa kujichora kwao, mavazi, nyimbo na hata mavazi pamoja na kubeba vitu vya asili ya mwafrika mfano kubeba chungu chenye moto kichwani.
![]()
Aina yao ya ushangiliaji wa mwanzo mwisho bila kujali timu yao inashambulia au inashambuliwa hata pale ilipokuwa nyuma kwa matokeo wao hawakuacha kushangilia. Walikuwa ni kiburudisho tosha kwa mashabiki wengine waliokuwepo uwanjani kutokana na burudani waliokuwa wanaitoa.
Shabiki wa Simba
![]()
Ahazi Sadock Mwembe huyu ni shabiki wa Simba kutoka Tunduma, Songwe. Ubunifu wake aliokuja nao kwenye uwanja wa Jamhuri Dodoma ulikuwa kivutio na kiburudisho tosha ukiachana na mambo mengine ya pembeni.
Kwanza huyu jamaa ametumia ghrama kubwa kutengeneza hivyo vitu unavyomuona navyo, msumeno umegharimu Sh. 25,000 hilo kombe alilobeba kichwani amefinyangiwa kwa 50,000 jamaa hakai kwenye majukwaa ya bei rahisi anakata tiketi za VIP jukwaa la VIP kwenye mchezo wa fainali ya ASFC tiketi zake ziliuzwa 20,000 achana na nauli ya kutoka Tunduma na kurudi, hotel, usafiri wa ndani na mambo mengine.
![]()
Kwa hiyo ukimuona shabiki analia baada ya timu yake kupoteza mechi huwa kuna mambo mengi ndani yake mbali na mapenzi kwa timu, ushindi pekee ndio huwa unalipa gharama zote hizo na kumfanya asahau kila kitu.
Ustaarabu wa mashabiki
![]()
Utaratibu uliotumiwa na mashabiki wa Dodoma na wengine waliosafiri kutoka maeneo mengine pia ulikuwa kivutio na ulionesha ustaarabu wa mtanzania halisi. Mashabiki walianza kuingia uwanjani kuanzia saa 2:00 asubuhi wakiwa kwenye mistari bila kuambiwa na mtu wala kushurutishwa.
Hakukuwa na kupishana kati ya mashabiki wenyewe wala mashabiki na jeshi la polisi, hakuna shabiki aliyepigwa hata kibao, mashabiki walijiongoza wenyewe na kila mmoja alikuwa mlinzi wa mwingine kuhakikisha utaratibu unafuatwa.
Hiki kitu ni mara chache kukiona katika maeneo mengine ya nchi hususan Dar es Salaam ambapo kila mtu angetaka kuleta ujanja wa kuja kachelewa halafu anataka kuwa wa kwanza kuingia uwanjani na huo ndio huwa mwanzo wa vurumai na poilisi kulazimika kutumia nguvu ya zaida ili kuleta utulivu. Katika hili HONGERENI mashabiki mliojitokeza kushudia mchezo wa fainali ya ASFC kwenye uwanja wa Dodoma.